Jumatatu , 2nd Dec , 2019

Mzee Meshuku Mapi Mukari almaarufu mzee Laibon, kutoka jamii ya kifugaji, mwenye umri wa miaka 102 na wake wapatao nane, watoto zaidi ya 60 na wajukuu zaidi 70, amesema kuwa licha ya kuwa na idadi kubwa ya watu nyumbani kwake, lakini wameweza kuishi kwa amani bila migongano yoyote.

Mzee Laibon, Mfugaji mwenye umri wa miaka 102, watoto zaidi ya 60 na wajukuu zaidi ya 70

Mzee Laibon ni Mkazi wa Kijiji cha Esilalei, wilayani Monduli, mkoani Arusha, anasema kuwa amelazimika kufungua Shule ambayo itaweza kuwa mkombozi kwa wajukuu zake na wale watoto wanaoishi jirani na eneo hilo, ambayo imechagiza hamasa ya elimu katika jamii hiyo ya kifugaji, ambayo kwa muda mrefu imekuwa nyuma katika masuala ya elimu.

Akizungumza na EATV, Mwalimu Abel Langa, ambaye ni mmoja ya walimu katika Shule iliyoanzishwa na Mzee Laibon, amesema muitikio wa elimu katika jamii hiyo, umeendelea kuwa mkubwa na hii imetoa hamasa kubwa ya elimu kwa jamii hiyo.

 Aidha katika hatua nyingine, familia ya Mzee Laibon, imeanza kufuata na kuabudu imani ya Kikristo na kuachana na baadhi ya mila potofu kama vile ukeketaji na unyanyasaji wa kijinsia.