Ijumaa , 11th Sep , 2020

Serikali imetoa onyo kwa wafanyabiashara nchini ambao bado wanaendelea kuingiza vibebeo vilivyopigwa marufuku kwa mujibu wa kanuni ya sheria za mazingira na kuwataka wafanyabiashara kuendelea kubadilisha fikra kwa kuwa Mpango uliopo ni kuondoa kabisa malighafi zote zenye madhara.

Mkurugenzi Mkuu (NEMC)Dk Samuel Gwamaka katika mahojiano na EATV ofisini kwake

Onyo hilo  limetolewa na Mkurugenzi Mkuu kutoka Baraza la Taifa la hifadhi na usimamizi wa Mazingira (NEMC)Dk Samuel Gwamaka kufuatia kuwepo kwa wafanyabiashara wachache wenye vitendo hivyo akibainisha kuwa kitu chochote cha kisichooza ni hatari kwenye mazingira.

"Tumekuwa tukitoa maonyo kila Mara lakini bado kuna wafanyabiashara wasio waaminifu wanatumia njia za panya kuingiza vibebeo vilivyopigwa marufuku na serikali kwa sasa tukikukamata tutakufungulia mashitaka na ukibainika kwa mujibu wa Sheria za nchi wachukuliwe hatua kali "-Dk Samuel Gwamaka.

Katika mahojiano na EATV  amezitaka halimashauri zote nchini kuhakikisha wanaweka  utaratibu wa kufanya utafiti juu ya aina za taka zinazozalishwa katika maeneo mbalimbali ili iwe  rahisi kuzisafirisha kwenda mahali husika.

"Nitumie fursa hii kutoa ushauri kuwa manispaa zote kufanya tafiti juu ya taka zinazozalishwa kwenye maeneo yao kwa kuwa nyingi hazikusanywi inavyostahili kutokana na changamoto mbali mbali baraza lipo na wataalamu wako hapa tuko tayari kuwaelekeza mbinu rahisi zenye gharama nafuu katika kuyalinda mazingira yetu"alisema Dk Gwamaka Mkurugenzi Mkuu NEMC.

Takataka zimetajwa kuwa fursa ambayo jamii inaweza kuitumia kwa kuzikusanya kwa aina ya makundi yake na kuzirejeleza hali inayoweza kuongeza kipato kwa mtu na taifa  kutokana na uwekezaji wa viwanda.