Jumamosi , 6th Jun , 2015

Rais Kikwete atuma salamu za rambirambi kuombeleza vifo vya zaidi ya watu 400 ambao wamepoteza maisha yao katika ajali ya boti ya kitalii, iliyozama katika Mto wa Yangtze mwanzoni mwa wiki hii.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Rais wa Jamhuri ya Watu wa China, Mheshimiwa Xi Jinping kuombeleza vifo vya zaidi ya watu 400 ambao wamepoteza maisha yao katika ajali ya boti ya kitalii, iliyozama katika Mto wa Yangtze mwanzoni mwa wiki hii.

Meli ya kitalii ya Eastern Star ilizama katika Mto wa Yangtze, karibu na mji wa Jianli, Jimbo la Kati la Hubei, Jumatatu usiku ikiwa na abiria 456 waliokuwa wanafanya safari ya kitalii ya siku 11 kutoka Nanjing kwenda Chongqing. Mpaka usiku wa jana, Ijumaa, Juni 5,2015, miili ya watu 369 ilikwishapatikana, watu 46 walikuwa hawajulikani walipo na 14 walikuwa wameokolewa.

Katika salamu zake za rambirambi, Rais Kikwete amemwambia Rais Jinping: “Nimepokea kwa mshtuko na masikitiko taarifa ya vifo vya mamia ya watu waliopoteza maisha yao katika ajali ya boti ya kitalii ya Eastern Star katika Jimbo la Hubei iliyotokea mwanzoni mwa wiki hii wakiwa katika safari kutoka Nanjing kwenda Chongqing.”

“Kwa hakika, haya ni maafa ya kitaifa. Kwa niaba ya Watanzania wenzangu, Serikali yangu na mimi mwenyewe, nakutumia wewe binafsi, Serikali yako na wananchi wote wa China salamu za dhati ya moyo wangu na naungana nanyi katika kuomboleza tukio hili la huzuni kubwa.”

Ameongeza Rais Kikwete katika salamu zake alizozituma usiku wa jana, Ijumaa, Juni 5, 2015: “Tanzania ikiwa nchi rafiki na China na Watanzania wote wanaungana na wenzao wa China kuwapa pole nyingi wote ambao wamepoteza wapendwa wao katika ajali hiyo.”

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
6 Juni, 2015