Jumamosi , 16th Dec , 2017

Rais wa Zimbabwe, Emmerson Mnangagwa ametaka wanachama wa Chama cha Zanu-PF kuachana na nyimbo za kumsifu na kuwataka watilie mkazo wimbo wa Taifa na nyingine zinazozungumzia ukombozi.

Mnangagwa amesema hayo katika mkutano wa chama hicho ambapo amewataka wanachama kutambua kuwa yeye ni Rais wa watu wote na wala si wa kikundi fulani.

Mkutano huo umemwidhinisha  Mnangagwa kuwa Mkuu Mpya wa chama na mgombea urais katika uchaguzi wa mwaka 2018. na kumvua rasmi uongozi aliyekuwa kiongozi mkongwe wa chama na Serikali ya Zimbabwe, Rais Robert Mugabe.

Rais Mnangagwa amesema wanachama wanapaswa kurekebisha uchumi ikiwa wanataka wawe na nafasi ya kushinda uchaguzi mkuu utakaofanyika mwakani.

Huu si wakati wa kutambiana kuwa kundi gani limeshinda bali kila mwanachama anapaswa kuzingatia mahitaji ya wananchi ambao wanataka maendeleo” amesema