Alhamisi , 17th Jul , 2014

Msajili wa mahakama kuu nchini Tanzania ametupilia mbali ombi la kituo cha sheria na haki za binadamu LHRC kutaka tozo ya shilingi bilioni 2.8 iliyotolewa na kampuni ya kufua umeme ya Dowans dhidi yao isisajiliwe kwa madai ya kuwa kinyume na sheria.

Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu LHRC Dkt Hellen Kijo-Bisimba.

Mkurugenzi mkuu wa kituo hicho Dkt Hellen Kijo-Bisimba, amesema hayo katika mahojiano na East Africa Radio ambayo jana iliripoti uwezekano wa kituo hicho kufungwa na shughuli zake kusitishwa moja kwa moja iwapo mahakama itakubali na kuisajili tozo hiyo.

Katika hoja ya msingi, LHRC inapinga kulipa kiasi hicho cha pesa kwa madai kuwa ni kikubwa mno na kipo kinyume na sheria kwani shauri walilofungua na ambalo limesababisha kuwpo kwa madai hayo ni lenye maslahi ya moja kwa moja kwa wananchi na kwa taifa.

Shauri hilo ni lile lililofunguliwa na mwandishi wa habari mkongwe Timothy Kahoho, Chama cha wanasheria wa Mazingira - LEAT pamoja na taasisi ya utetezi wa huduma bora za afya ya SIKIKA, ambao kwa pamoja walikuwa wanaitaka mahakama kuu isikubali kusajili tozo hiyo.

Kwa mujibu wa Dkt Bisimba, hatua yoyote ya kung'ang'ania taasisi hiyo ilipe tozo hiyo ni sawa na kutangaza kukifunga kituo hicho, hatua anayodai kua itaaathiri takribani Watanzania elfu kumi na tano ambao kituo hicho kimefungua kesi kwa niaba yao na zinazoendelea katika mahakama mbali mbali nchini.