Alhamisi , 3rd Dec , 2015

Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii kwa kushirikiana na ofisi za mikoa mbalimbali nchini inatarajia kuendesha zoezi la ugawaji wa dawa kwa ajili ya magonjwa ambayo yalikuwa hayapewi kipaumbele.

Mratibu wa Mpango wa Taifa wa Kudhibiti Magonjwa yaliyokuwa hayapewi kipaumbele Dk Upendo Mwingira (kushoto)

Kauli hiyo imetolewa jana jijini Dar es salaam na mratibu wa kitaifa wa mpango wa taifa wa kudhibiti magonjwa ambayo yalikuwa hayapewi kipaumbele Dkt. Upendo Mwingira wakati wa semina ya wahariri wa vyombo vya habari mbalimbali nchini.

Amesema kuwa zoezi hilo linatarajiwa kufanyika kuanzia hivi karibuni ambapo dawa za magonjwa hayo ni minyoo, matende na mabusha zitatolewa bila malipo kwa wananchi wote.

Dkt. Mwingira amesema kuwa dawa hizo zitatolewa kwenye hospitali, vituo vya afya, zahanati masoko, vituo vya Basi, treni , shuleni, mashirika ya umma, nyumba za ibada, kambi za jeshi na Wizarani.

Ameongeza kuwa walengwa ni wananchi wote wenye umri wa miaka kuanzia mitano hadi kuendelea. Alifafanua kwamba dawa hizo humezwa kila mwaka.

Dkt. Mwingira alisema kampeni hiyo itaanza katika jiji la Dar es Salaam kuanzia Desemba mwaka huu na mikoa ambayo itaambatana na kampeni hiyo ni Katavi, Rukwa, Lindi, Mtwara, Singida, Dodoma na Pwani. Mikoa iliyobakia kampeni hiyo itafanyika kwa awamu kati ya Januari na Februari mwaka huu.

Aidha Dkt. Mwingira amesisitiza kuwa dawa zitakazotolewa ambazo ni Albendazolena Ivermectin hazina madhara yoyote na kuongeza kuwa ni vema wananchi wakatumia fursa hiyo kujipatia tibakinga.