Jumapili , 22nd Sep , 2019

Waziri wa Elimu, Prof. Joyce Ndalichako, amewataka wanafunzi waliosoma Shule binafsi kwa ufadhili na hawakujaza vizuri taarifa zao za uombaji wa mkopo, wawasiliane na Bodi ya Mikopo, iangaliwe kama kuna uwezekano wa kupata fursa hiyo.

Waziri Ndalichako amesema hayo leo Septemba 22, 2019, katika ibada ya Jumapili ya uzinduzi wa juma la elimu katika Kanisa la KKKT Dayosisi ya Mashariki na Pwani, ambapo amesema ipo dhana kuwa waliosoma shule za bianfsi hawawezi kupata mikopo, jambo ambalo si sahihi.

"Kama kuna Mwanafunzi yeyote ambaye alikuwa anasoma shule binafsi kwa ufadhili, na katika fomu kuomba mkopo, alisahau kuweka hiyo taarifa awasiliane na Bodi ya Mikopo,ili tuone namna ya kumwezesha, kuna wakati wanafunzi wanakosa mikopo kwa kutojaza kwa usahihi." amesema Ndalichako
 
Amesema kuwa Serikali ipo tayari kuwapatia mikopo wanafunzi wote waliosoma kwa ufadhili, kutokana na wao kushindwa kujilipia gharama za masomo, ili mradi wahakikishe wanajaza taarifa sahihi.