Jumapili , 4th Nov , 2018

Wizara ya Mambo ya nje na Uhusiano wa Kimataifa imetoa msimamo wake juu ya sakata la Mkuu wa Mkoa wa Dar es saalam dhidi ya ushoga katika mkoa wake aliyoianzisha wiki iliyopita.

Mkuu wa Mkoa wa Dar es salaam, Paul Makonda akiwa na viongozi wa dini leo wakati wa ibaada ya kukemea vitendo vya ushoga jijini Dar es salaam.

Taarifa ya wizara hiyo iliyotolewa leo, Jumapili Novemba 4, serikali imekumbusha na kusisitiza kuwa itaendelea kuheshimu mikataba yote ya kimataifa inayohusu haki za binadamu ambayo imesaini na kuiridhia.

Taarifa hiyo imesema kuwa, “Wizara ya Mambo ya Nje kwa niaba ya Serikali inapenda kuwajulisha wananchi na jumuiya ya kimataifa kupitia vyombo vya habari vya ndani na nje ya nchi kuhusu masuala ya ushoga yaliyoongelewa na mkuu wa mkoa wa Dar es salaam,

Imeongeza kuwa  “Jamhuri ya Muungano wa Tanzania inaendelea na itaendelea kuheshimu na kulinda haki hizo kama zilivyo katika Katiba na serikali ya Tanzania ingependa kufafanua kwamba hayo ni mawazo yake (Makonda) na si msimamo wa serikali".

Katika mkutano wake na waandishi wa habari Oktoba 31, 2018, Makonda alitangaza kampeni ya kukabiliana na vitendo vya ushoga katika jiji la Dar es salaam, ambapo aliunda kamati ya watu 15 kwa ajili ya kupambana na wanaojihusisha na ushoga, wanaotapeli wengine kwa kutumia mitandao wakijifanya ni viongozi maarufu nchini.