Alhamisi , 11th Apr , 2019

Serikali kupitia Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto imetoa tahadhari ya kuwepo kwa ugonjwa wa Dengue nchini ambao umebainika katika mikoa ya Dar es salaam na Tanga.

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile akitoa tahadhari kuhusu kuzuka kwa ugonjwa wa Dengue nchini. Kushoto ni Mganga mkuu wa Serikali Prof. Mohammed Kambi.

Akitoa tahadhari hiyo mbele ya waandishi wa habari jijini Dodoma leo, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Faustine Ndugulile amesema hadi kufikia April 2, 2019 kati ya watu 470 waliopimwa, wagonjwa 307 wamethibitishhwa kuwa na virusi vya ugonjwa wa Dengue, na kati ya hao 252 ni kutoka Dar es salaam na 55 ni kutoka Tanga.

"Dalili za ugonjwa huo kuwa ni homa ya ghafla, kuumwa kichwa hususani sehemu za macho, maumivu ya viungo na uchovu. Dalili hizi huanza kujitokeza kati ya siku 3 hadi 14 tangu mtu alipoambikizwa  virusi vya ugonjwa huu", amesema Dkt. Ndugulile.

Ugonjwa wa homa ya Dengue unasababishwa na virusi vinavyoenezwa na mbu wa aina ya “Aedes” ambao ni weusi wenye madoadoa meupe yenye kung’aa, ambapo hawa huwa na tabia ya kuuma zaidi wakati wa mchana hasa wakati wa asubuhi jua linapochomoza na jioni jua linapozama.