Jumapili , 28th Jul , 2019

Mashirika Yasiyo ya Kiserikali kwa Kanda ya Kasikazini yaliyosajili awali chini ya sheria nyingine lakini zinafanya kazi za kijamii, yametakiwa kusajili kwa sheria ya NGOs kama ilivyofanyiwa marekebisho na sheria Na.3 ya Mwaka 2019.

NGOs

Akizungumza na vyombo vya  habari  leo  Mkoani Kilimanjaro, Msemaji wa Wizara ya Afya Idara Kuu Maendeleo ya Jamii Bw. Erasto Ching’oro amesema zoezi hilo litafanyika katika Ofisi za Mkuu wa Mkoa Kilimanjaro kuanzia tarehe 29, July hadi tarehe 6 Augosti 2019 ili kutoa fursa kwa wadau wa Mashirika yaliyoko Mikoa ya Kasikazini kufanya usajili kwa haraka.

"Sheria inayataka Mashirika hayo kujisajili katika Sheria ya NGOs kwa kipindi cha miezi miwili hivyo huu ni wakati wa Mashirika kujitahimini yako wapi ili yaweze kufanya uamuzi sahihi kabla ya kipindi kilichotolewa na Sheria hii kupita’’, amesisitiza Bw. Ching’oro.

Amesema usajili huo unafanyika kwa mikoa ya Kanda ya Kaskazini yenye mikoa ya Tanga, Kilimanjaro, Arusha na Manyara na kutoa wito kwa Mashirika yaliyopo katika Mikoa hiyo kufanya usajili huo akiongeza kuwa zoezi hili linafanyika bila malipo kwa Mashirika yanayouhisha usajili lakini Mashirika yanayojisajili mara ya kwanza yanatoa malipo kwa ajili ya huduma hiyo.

Zoezi hili la usajili limeanza tangu tarehe 10 mwezi huu Jijini Dar es Salaam ambapo asilimia 80 ya NGOs zilizoko Kanda ya Mashiriki zimefanya usajili wake na zoezi la usajili linaendelea kwa kipindi cha miezi miwili kama ilivyo matakwa ya sheria.