Jumatatu , 9th Sep , 2019

Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini Patrobas Katambi, amezungumzia mahusiano yake na Mbunge wa Mbeya Mjini Joseph Mbilinyi (Sugu), ambapo amempongeza kwa maamuzi ya kuoa kwa madai ya kwamba ameamua kuchagua tabia njema na si mwonekano wa mtu.

Mbunge wa Mbeya Mjini Joseph Mbilinyi na Mkuu wa Wilaya ya Dodoma Mjini Patrobas Katambi.

Akizungumza na EATV&EA Radio Digital Katambi amesema kuwa, licha ya kumpongeza lakini amemtaka kuachana na mambo yasiyokuwa na tija kwa wananchi wake na badala yake afanye vitu ambavyo ni bora kama alivyoamua kuchuja na kuchagua mmoja kati ya wale mamilioni aliokuwa nao  na kupata mke aliye mwema.

''Sugu si unajua alikuwa mzee wa Toto nyingi, hata kuoa kwake naona hakuangalia sana sura alijikita nadhani kwenye tabia, lakini sasa kwa umakini huo alioutumia kuchuja katika kuoa  basi ajichuje kwenye siasa,  afanye siasa zenye tija na maendeleo zitakazosaidia Taifa na watu wa Mbeya kupunguza walau yale maneno yasiyo na tija, kwahiyo  kama alishauriwa akaona hilo akaweza kulifanya na watu tukampongeza  basi na kwenye siasa ajitahidi napo tutampongeza'' amesema DC Katambi.

Mbunge Sugu alifunga ndoa siku ya Agosti 31, 2019 na aliyekuwa mpenzi wake wa muda mrefu Happiness Msonga, sherehe iliyohudhuriwa na viongozi mbalimba wa vyama vya siasa.