Jumatatu , 7th Mar , 2016

Tanzania inatarajia kunufaikia kiuchumi na mkutano wa biashara utakaofanyika katika ukumbi wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam keshokutwa.

Mkutano huo utawakutanisha wafanyabiashara wa hapa nchini na wale kutoka nchini Vietnam, mkutano utakaofanyika kufuatia ziara ya rais wa nchi hiyo mhe. Truong Tan Sanga atakayetembelea nchini hivi karibuni.

Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji mhe. Charles Mwijage ametoa wito huo jijini Dar es Salaam leo, katika mkutano wa pamoja baina ya wizara hiyo na Taasisi ya Sekta Binafsi nchini TPSF, na kufafanua kuwa mkutano huo unaoratibiwa kwa ushirikiano wa kituo cha Uwekezaji nchini TIC na TPSF utatoa fursa pana ya jinsi Tanzania inavyoweza kujifunza kutokana na mafanikio ya kiuchumi yaliyofikiwa na taifa la Vietnam.

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa TPSF Dkt Godfrey Simbeye, amesema sekta binafsi nchini itatumia mkutano huo kujifunza mbinu zilizotumiwa na taifa la Vietnam hadi kufikia mafanikio hayo ya kiuchumi, licha ya Tanzania kuwa na ardhi kubwa yenye fursa nyingi za kiuchumi.

Mkurugenzi wa kituo cha uwekezaji nchini amesema kufanyika kwa mkutano huo ni sehemu ya juhudi zinazofanywa na kituo hicho za kuvutia uwekezaji kutoka nje na hasa pato la fedha za kigeni kupitia miradi ya uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje.