Ijumaa , 8th Jul , 2016

Waziri wa Nishati na Madini, madini Mhe. Sospeter Muhongo, amesema kuwa Serikali ya Uganda itajenga kiwanda cha kuchakata mafuta ghafi kwenye eneo la Kabaale wilani Hoima nchini humo.

Waziri wa Nishati na Madini, madini Mhe. Sospeter Muhongo.

Prof. Muhongo amesema hayo baada ya kutembelea eneo hilo nchini Uganda wakati wa vikao wa kujadili michakato wa ujenzi wa bomba la mafuta kutoka Kabaale hadi katika bandari ya Tanga.

Amesema serikali ya Uganda imetoa jumla ya asilimia 40 ya Hisa ya kiwanda hicho kwa nchi tano za Afrika Mashariki zenye thamani ya zaidi ya dola milioni 150 za kimarekani ikiwa ni sawa na hisa nane kwa kila mmoja.

Ujenzi wa Bomba hilo kutoka nchini Uganda hadi Tanzania Mkoani Tanga utagharimu dola bilioni 3.55 na litakuwa na urefu wa kilimeta 1443 na uwezo wa kusafirisha mapipa laki mbili ya mafuta kwa siku.

Katika hatua nyingine ujumbe wa Tanzania na ule wa Uganda katika ujenzi wa bomba la mafuta umetembelea eneo la ziwa Albert na kuona visima vilivyochimbwa tayari kwa uzalishaji wa mafuta ghafi ambapo inakadiriwa kuwa na mapipa bilioni sita.