Jumatano , 5th Mei , 2021

Rais wa Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta ametoa wiki mbili kwa ajili ya kushughulikiwa tatizo la mrundikano wa mahindi  katika eneo la mpakani ili biashara ziendelee kama awali.

Rais wa Kenya Mhe. Uhuru Kenyatta

Rais Uhuru ametoa wiki mbili hizo leo wakati akiongea katika mkutano wa wafanyabiashara wa Kenya na Uganda, uliofanyika leo, ambapo ameainisha masuala mawili ambayo anataka yafanyiwe kazi kabla ya mawaziri wa nchi hizo mbili kukutana kwa ajili ya kutatua changamoto za kibiashara zilizopo baina yao.

“Mimi nitaje mambo mawili nayotaka yatendeke na hii ninataka yafanyike wiki hii na wiki ijayo, kwanza ni mawaziri ambao wanahusika muende mtatue msongamano ambao upo Taveta , Holili,  na pale Namanga magari yaweze kutembea, kama ni certificate za covid- 19 mawaziri wa afya wajue namna ya kufanya certificate ikitolewa Tanzania iwe sawa na aingie Kenya na vinginevyo” amesema Rais Kenyatta

Rais Uhuru ameongeza, “Pili ni mahindi ambayo yamelala mpakani, waziri mimi nakupatia wiki mbili mahindi yote yawe yamefunguliwa na maneno yaishe kwasababu hatutaki kuumiza watu wetu,” 

Awali akiongea kwenye mkutano huo Rais Kenyatta amewataka wawekezaji watanzania kuwa na uhuru  kuwekeza nchini Kenya  bila kusumbuliwa na masuala ya visa  wala vibali vya kazi ila wanao wajibu wa kufuata sheria na kanuni zilizowekwa.