Jumamosi , 16th Jan , 2016

Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kimapata ushindi katika uchaguzi wa umeya wa manispaa za Ilala na Kinondoni jijini Dar es salaam.

Boniphace Jacob, Meya mpya wa Kinondoni

Chama cha Demokrasia na Maendeleo CHADEMA kimapata ushindi katika uchaguzi wa umeya wa manispaa za Ilala na Kinondoni jijini Dar es salaam.

Katika manispaa ya Kinondoni madiwani wa halmashauri hiyo wamemchagua Boniphace Jacob ambaye ni diwani wa Ubungo kuwa Meya wa manispaa hiyo baada ya kupata kura kura 38 dhidi ya mgombea Benjamin Sitta (CCM) aliyepa kura 20.

Akitangaza matokeo hayo kaimu mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni Bwana Aron Kagurumjuli amemtangaza rasmi Bwana Boniphace Jacob kuwa Meya manispaa ya kinondoni kutokana na ushindi huo ambapo kura halali zilikuwa 58 na hakuna kura iliyoharibika.

Madiwani hao pia wamemchagua diwani wa kata ya Tandale Jumanne Amir Mbunju (CUF) kuwa Naibu Meya kuwa kura 38 dhidi ya kura 19 kutoka kwa mpinzani wake kutoka CCM.

Katika Manispaa ya Ilala, Charles Kwiyeko (CHADEMA) amechaguliwa kuwa Meya wa manispaa ya hiyo na Omary Kumbilamorto (CUF) kuwa naibu Meya.

Kwiyeko ambaye ni diwani wa Bonyokwa amemshinda mgombea wa CCM Herry Kessy kwa kupata kura 31 kwa 0 sawa na kura ambazo pia Naibu Meya Omary Kumbilamoto amezipata.

Katika uchaguzi huo, madiwani wa Chama Cha Mapinduzi licha ya kuhudhuria kikao hicho, walisusia uchaguzi huo muda mfupi kabla kura hazijapigwa, hali iliyomlazimu msimamizi wa uchaguzi huo kuendelea na mchakato kwa kuwa akidi ilikuwa imetimia.

Awali uchaguzi katika manispaa hizo uliahirishwa mara kadhaa kutokana na utata wa ushiriki wa wabunge wa viti maalum kutoka Zanzibar kabla waziri wa TAMISEMi George Simbachawene hajatoa maamuzi kuwa wabunge wao hawakustahili kushiriki kama wajumbe katika manispaa hizo kwa kuwa suala la halamshauri siyo la muungano.

Charles Kwiyeko, Meya mpya wa Ilala