Alhamisi , 31st Jul , 2014

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC) kimesema kumekuwa na ongezeko kubwa la ukiukwaji wa haki za binadamu nchini ambapo kwa mwaka huu watu wapatao 320 wameuwawa ikilinganishwa na watu 303 mwaka jana.

Mkurugenzi mkuu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu - LHRC Dkt Hellen Kijo- Bisimba.

Mtafiti wa LHRC Bw. Pasiance Mlowe amesema hayo leo jijini Dar es Salaam na kufafanua kuwa wengi kati ya watu hao wameuawa kutokana na imani za kishirikina.

Kwa mujibu wa Mlowe, ongezeko kubwa la watu kujichukulia sheria mikononi, mauaji ya imani za kishirikina na mauaji ya watu wenye ulemavu yanatokana na kukosekana kwa elimu ya haki za binadamu katika mfumo wa elimu nchini.

Kwa upande wao wananchi waishio maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam wakiongea na East Africa Radio wamesema kutokutenda haki kwa wasimamiaji wa sheria ikiwemo mahakama na polisi kumeongeza hali ya wananchi kujichukulia sheria mkononi ambapo wameitaka serikali kutoa elimu kuhusu haki za binadamu wanaojichukulia sheria mkononi kudhibitiwa.

Wakati huo huo, watuhumiwa 25 wa matukio ya ulipuaji wa mabomu katika Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasit, mkutano wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo Chadema, Bar ya Arusha Night Park , Mgahawa wa Vama na umwangiaji wa tindikali kwa baadhi ya watu, wanatarajia kufikishwa Mahakamani hapo kesho.

Akizungumza na waandishi wa habari leo, jijini Arusha Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Liberatus Sabas amesema katika tukio la ulipuaji bomu Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi Olasiti lilitokea Mei 5 mwaka 2013 ambapo watu zaidi ya 16 walijeruhiwa na watatu kufariki dunia,

Kamanda Sabas amesema tukio la kurushwa bomu nyumbani kwa Sheikh Sudi Aly Sudi lilitokea Julai 3 mwaka huu na watuhumiwa wengine kumi watafikishwa mahakamani kwa tukio la kupatikana na mabomu saba nyumbani Julai 21 mwaka huu, huku watuhumiwa watatu, watafikishwa mahakamani kwa kuhamasisha vitendo vya kigaidi kupitia mtandao wa kijamii