Jumanne , 6th Jan , 2015

VIONGOZI wapya wa Serikali za Mitaa, katika Jiji la Arusha, wameilalamikia serikali kukosa ofisi za kufanyia kazi na kusababisha kutembea na mihuri ya kazi ndani ya makoti yao wakati wa kufanya kazi za wananchi wao.

Mkurugenzi wa Jiji la Arusha Juma Iddi

Wakizungumza leo kwa nyakati tofauti ndani ya mkutano ulioandaliwa na Jiji la Arusha kwa lengo la kuwafahamisha majukumu yao muhimu katika nafasi hizo, Edward Sambai na Mohamedy Omari, wamesema inasikitisha kuona serikali inawathamini Madiwani ila wao wenyeviti wa serikali za mitaa wanadharauliwa.

Wamesema kitendo cha kukosa ofisi kinawalazimu kutembea na mihuri ya kazi kwenye makoti yao, huko mtaani jambo ambalo siyo sahihi na linawanyima hadhi yao.

Wamemwomba Mkurugenzi wa Jiji hilo Juma Iddi afanye ziara ya kutembea kwenye kata zote 25 zenye mitaa 154 ili washirikiane kuona maeneo gani ya wazi yanafaa kujenga ofisi zao.

Naye Mkurugenzi wa Jiji la Arusha, Juma Iddi akijibu malalamiko hayo, amesema kuwa suala hilo lina ukweli, lakini wanaweza kutumia kwa muda ofisi za Kata na wakati huo huo, atazunguka kwenye maeneo yao ili washirikiane kuona kama wataweza kujenga ofisi.

Aidha amewaonya viongozi hao kuwa makini katika utendaji wao wa kazi kwa kuepuka kutoa huduma kwa ubaguzi wa vyama na itikadi za dini na vyama vyao.

Wakti hhuo huo Viongozi wa serikali za mitaa katika manispaa ya Dodoma waliochaguliwa kwenye uchaguzi uliofanyika Desemba 14 mwaka jana wameapishwa jana na kusomewa majukumu yao ya kazi.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukamilika kwa zoezi la kuwaapisha viongozi hao, Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Augustino Kalinga, amesema zoezi hilo limefanyika kwa mafanikio makubwa.. kwa wenyeviti wa seriklai za mitaa, vitongoji na vijiji pamoja na wajumbe wao kuapishwa tayari kwa kutekeleza majukumu yao.