Jumapili , 2nd Jun , 2019

Jumla ya vyama nane vya upinzani nchini vimeadhimia kutoshiriki uchaguzi wa marudiano endapo Tume ya taifa ya Uchaguzi (NEC) haitofuatilia malalamiko yao waliyowasilisha mahakamani kuhusu wasimamizi wa chaguzi mbalimbali ambao ni wakurugenzi wa halmashauri.

Baadhi ya Bendera za vyama vya upinzani.

Akisoma tamkoa hilo, Mwenyekiti wa chama cha UPDP, Fahmi Dovutwa, kwa niaba ya vyama hivyo ambavyo ni pamoja na ACT Wazalendo, CCK, CHADEMA, CHAUMMA, DP,NCCR na NLD, amesema, "tumekubaliana kuwa vyama vyote 8 kutoshiriki huu uchaguzi wa marudio kwani kufanya hivyo ni sawa na kubariki 'dharau' kwa mahakama inayoonyeshwa na Tume ya Taifa ya uchaguzi".

"Tunaitaka Tume ya Taifa ya Uchaguzi kutumia mamlaka yake iliyopewa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Ibara ya 74 (15) (e) na kuteua wasimamizi wa uchaguzi huu wa marudio mara moja", amesema Dovutwa.

Hayo yanajiri ikiwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imetangaza kufanyika kwa uchaguzi mdogo wa marudio katika kata 32 unaotarajiwa kufanyika Juni 15, 2019.