Jumatano , 21st Feb , 2018

Idara ya Uhamiaji nchini inawashikilia watanzania 9, ambao ni  wafanyakazi wa Chuo Kikuu cha Kimataifa cha Kampala(KIU) jijini Dar  es Saalam kwa madai ya kuzuia maofisa wa idara yao kutofanya kazi yao walipofika chuoni hapo.

Msemaji wa  Idara ya Uhamiaji Ally Mtanda amesema watu hao tisa wamekamatwa  jana kwa tuhuma za kuzuia maofisa wa idara hiyo wasitimize  majukumu yao na kwa sasa wanawahoji. 

"Watu hao baada ya maofisa wetu jana kufika pale KIU waliamua kuwazuia kwa kufunga milango ili tusipate nafasi ya kufanya kile ambacho kimetupeleka,"amesema.

Kukamatwa kwa watu hao kunafanya idadi ya wanaowashikiliwa na Idara ya Uhamiaji kufikia 48.

"Idara ya Uhamiaji inaendelea kuwahoji na kati ya hao wanaoshikiliwa wapo raia wa Nigeria watano, raia wa Congo mmoja, raia wa Uganda 30, raia wa Kenya 3 pamoja na hao raia wa Tanzania 9,"amesema.

Amefafanua Idara ya Uhamiaji itaendelea kukagua vyuo mbalimbali  nchini kwani ni agizo la Wizara ya Elimu, Sayansi na  Teknolojia.