
Majaji 6-3, walibatilisha amri ya mahakama ya chini iliyoitaka serikali kumpa mhamiaji "fursa" ya kuwaambia maafisa ni hatari gani anayoweza kukabiliana nayo anapohamishwa hadi nchi ambayo si yake.
Majaji watatu wa mahakama ya kiliberali walipinga uamuzi wa wengi, wakisema ni "kuidhinisha uvunjaji wa sheria".
Kesi hiyo inawahusisha wahamiaji wanane kutoka Myanmar, Sudan Kusini, Cuba, Mexico, Laos na Vietnam, waliofukuzwa mwezi Mei kwa ndege inayosemekana kuelekea Sudan Kusini.
Jaji wa Wilaya ya Boston nchini Marekani, Brian Murphy, aliamua kwamba kuondolewa kwao kumekiuka agizo alilotoa mwezi Aprili kuwa wahamiaji lazima wapate fursa ya kujitetea kwamba wanaweza kuteswa au kuuawa ikiwa watahamishwa hadi nchi tofauti - hata kama rufaa zao zingine za kisheria zimeshindwa.
Uamuzi huo ni ushindi mwingine kwa rais wa Republican katika harakati zake za kufukuzwa kwa wahamiaji.
Mwezi uliopita, Mahakama ya Juu Zaidi ilimruhusu Trump kusitisha Hadhi ya Ulinzi ya Muda kwa raia wa Venezuela, na kuathiri takriban wahamiaji 350,000.
Katika uamuzi mwingine mwezi Mei, majaji walisema rais anaweza kusitisha kwa muda mpango wa kibinadamu ambao umeruhusu karibu wahamiaji nusu milioni kutoka Cuba, Haiti, Nicaragua na Venezuela kukaa Marekani kwa miaka miwili.