Jumatano , 5th Aug , 2015

Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania anayemaliza muda wake Anna Makinda ametoa wito kwa wakulima wa kanda ya Nyanda za juu Kusini kuongeza tija kwenye uzalishaji wa mzao ili kukidhi soko la kimataifa katika nchi za kusini mwa Afrika.

Spika wa Bunge la Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania anayemaliza muda wake Anna Makinda.

Mikoa ya Mbeya, Njombe, Iringa, Rukwa, Katavi na Ruvuma ni maarufu kwa jina la The Big Six hapa nchini kwa kuwa kinara wa uzalishaji wa mazao mbalimbali ya chakula na biashara yakiwemo Mahindi.

Akizungumza na chombo hiki Spika Makinda wakati wa ufunguzi wa maonyesho ya sherehe za wakulima Nanenane zinazofanyika kikanda mkoani Mbeya amesema kuwa kupitia uwanja wa kimataifa wa Songwe wakulima wanatakiwa kuutumia vyema uwanja huo kwa kuongeza uzalishaji ili kukidhi soko la kimataifa.

Kwa muda mrefu Tanzania imekuwa mkombozi kwa baadhi ya mataifa barani Afrika katika masuala ya chakula.

Lakini pamoja na hali hiyo changamoto pekee inabaki kuwa ni soko la uhakika ambalo linachangia baadhi ya wakulima kukata tamaa ya kuendelea na kilimo.

Kwa upande mwingine Chama cha Wakulima TASO kinataja changamoto ya uchakachuaji wa pembejeo kuwa kikwazo cha wakulima kushindwa kufikia malengo.