Jumamosi , 8th Dec , 2018

Waziri Mkuu wa 5 wa Tanzania, Joseph Warioba amefunguka juu ya tarehe 9 Disemba, siku ya ambayo Tanzania imekuwa ikisheherekea kupatikana kwa uhuru, ambapo ameeleza kwa wakati huo kuendesha nchi ilikuwa ni kitu kigumu sana kwa sababu kulikuwa na wasomi wachache.

Waziri Mkuu wa 5 wa Tanzania, Joseph Warioba.

Kwa mujibu wa Warioba ambaye kwa sasa ana miaka 78, wakati Tanganyika inapata uhuru yeye alikuwa na miaka 21 na kwa wakati huo nchi nzima ilikuwa na wahandisi wawili tu.

"Nakumbuka nilikuwa kijana wakati ule, na tulikuwa kwenye mapambano ya kupata uhuru, na tulishangazwa sana kuona bendera ya mkoloni inashushwa na bendera yetu ya Tanganyika inapanda, na baada ya hapo Mwalimu Nyerere alitushinikiza tufanye kazi kwa bidii." Amesema.

"Wakati tunapata uhuru kulikuwa na ubaguzi, waafrika tulikuwa tunaonekana ni watu wa hali ya chini, lakini siku hiyo tukaanza kujiona ni binadamu kama binadamu wengine." Ameongeza Warioba.

"Ni kweli wakati ule kulikuwa na wasomi wachache sana, mfano wahandisi nchi nzima walikuwa wawili tu na ukija kwenye taaluma nyingine walikuwa ni wachache tu japo mipango ilishaanza kuwepo ya kuwa na wasomi, ndiyo maana miezi miwili kabla ya uhuru kikafunguliwa chuo kikuu." Amesema.

Ameongeza kuwa kuhusu usafiri kipindi kile hali ilikuwa ngumu sana, ukilinganisha na sasa hivi, ambapo tumeendelea sana, kila kona kuna lami maeneo na yanafikika kwa urahisi.

Disemba 9, Tanzania inaadhimisha miaka 57 ya uhuru, ambapo Rais Magufuli licha ya kuwasihi watanzania kuendelea kufanya kazi pia aliamuru kiasi cha fedha kilichopangwa kutumika kwenye maadhimisho hayo kikatumike kujenga hospitali ya Uhuru Jijini Dodoma pamoja na kutangaza kuwasamehe wafungwa 1,076.