Jumatano , 24th Sep , 2014

Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu nchini Tanzania (LHRC) kimesema kumekuwepo na uelewa mdogo kwa watanzania juu ya mchakato unaoendelea wa kutengeneza Katiba mpya na hivyo kuleta hofu iwapo wananchi wataweza kuipitisha wakati wa kutoa maoni.

Mkurugenzi Mkuu wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu Dkt Hellen Kijo-Bisimba.

Mkurugenzi wa LHRC Dk. Hellen Kijo-Bisimba amesema hayo leo jijini Dar es Salaam wakati alipokuwa akitoa majumuisho ya kampeni waliyoiita Gogota yenye lengo la kusambaza uelewa wa rasimu ya pili ya Katiba kwa wananchi na kuwahamasisha kushiriki katika mchakato huo na kufuatilia bunge Maalum la Katiba.

Hata hivyo Dk. Kijo-Bisimba ameelezea kusikitishwa kwake na vitendo vya baadhi ya viongozi wa ngazi za juu katika mikoa waliyopita kuwazuia kutoa elimu ya uelewa kwa wananchi hao kwa madai kwamba ni kwa maslahi yao binafsi ama ya chama chao.

Wakati huo huo, Manispaa ya Ilala jijini Dar es salaam nchini Tanzania imetenga shilingi bilioni 2.9 kwa ajili ya ujenzi wa barabara katika manispaa hiyo ambapo kati ya fedha hizo shilingi bilioni 1.5 zimetoka mfuko wa barabara na shilingi bilioni 1 zimetoka katika halmashauri hiyo.

Hayo yameelezwa jijini Dar es salaam na Afisa uhusiano wa manispaa hiyo Bi. Tabu Shaibu wakari alipokuwa akieleza mpango mkakati wa manispaa hiyo katika ujenzi wa miundo mbinu yake.

Amesema lengo ni kuhakikisha kwamba ujenzi huo wa barabara unasaidia kupunguza msongamano wa magari sambamba na kuboresha njia ambazo kwa sasa zimeharibika kutokana mvua zilizonyesha.