Jumanne , 10th Mei , 2022

Kamishna wa Polisi Jamii Tanzania, Mussa Ally Mussa, amesema kuwa mkoa wa Kagera bado una idadi kubwa ya matukio ya mauaji na kwamba katika kipindi cha miezi mitatu kuanzia Januari hadi Machi mwaka huu, yametokea wastani wa mauaji kati ya watu 30 hadi 40.

Kamishna wa Polisi Jamii Tanzania, Mussa Ally Mussa

Kufuatia kukithiri kwa vitendo vya mauaji, ubakaji na ulawiti, Kamishna huyo pamoja na timu yake wamefika katika mkoa wa Kagera na kufanya kikao na uongozi wa mkoa, madiwani, watendaji wa vijiji, mitaa na Kata kutoka katika wilaya ya Bukoba ili kuweka mipango thabiti itakayosaidia kukabiliana na vitendo hivyo vya uhalifu.

"Kipindi cha miezi mitatu tu utagundua kwama wananchi si chini ya 40 wameuawa kama rate ndiyo hiyo halafu iende mwaka mzima utakuja kukuta ni zaidi ya watu 100 wameuawa," amesema Kamishna Mussa

Kamishna huyo amesema kuwa idadi ya watu wanaouawa katika mkoa wa Kagera bado ni kubwa, na kwamba jeshi la polisi haliwezi kuyafumbia macho.