Ijumaa , 20th Mei , 2016

Umoja wa Wazee wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Jijini Mbeya wamewalalamikia wakuu wa mikoa na wilaya wakisema hawajawajibika ipasavyo kusimamia huduma ya matibabu bure kwa wazee.

Mkuu wa Mkoa wa Mbeya Amos Makalla

Wazee hao wamebainisha hayo kwenye kikao chao na wanahabari mkoani Mbeya wakisema pamoja na serikali kuweka sera ya wazee kupata matibabu bure bado hakujawa na jitihada thabiti za usimamizi.

Mmoja wa wazee hao Kikeke A. Kikeke, amesema wakuu wa mikoa na wilaya wanapaswa kufuatilia kwa karibu kuhakikisha iwapo sera hiyo inasimamiwa lakini wamebaki kuzungumzia suala hilo wakiwa mbali na vituo vya kutolea huduma za afya.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Umoja hu,o Isakwisa Mwamburukutu, amesema huduma ya matibabu bure kwa wazee imekuwa ikiishia kwa kuchunguzwa na madaktari lakini dawa wanaambiwa wakanunue kwenye maduka ya watu binafsi.

Mwamburukutu amesema kutokana na kuhitajika kujinunulia dawa,wazee wamekuwa wakishindwa kupata matibabu na hivyo kusababisha waione sera husika kama ya kisiasa kwa kuwa haitekelezwi.

Ameiomba serikali kutumia kasi ya Rais Dkt. John Magufuli, kuliwekea mkazo suala la matibabu kwa wazee ili jamii hiyo iweze kunufaika na mikakati ya serikali ya kuboresha maisha ya kila mwananchi.