Jumatano , 18th Mei , 2016

Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Juma Ali Juma, amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imo katika mpango mkakati wa kuimarisha sekta nzima ya kilimo cha umwagiliaji ili kuhakikisha uzalishaji unaongezeka hasa mpunga.

Moja ya mashamba ya mpunga yanayotumia kilimo cha umwagiliaji

Akielezea hali halisi ya hali ya Chakula Zanzibar mara baada ya kufungua semina ya wadau wa kilimo Tanzania, iliyoandaliwa na shirika la Kimataifa, linalosimamia maendeleo ya Kilimo Duniani FAO, amesema Zanzibar ina eneo kubwa la kufanya kilimo tofauti tofauti na kuongeza uzalishaji.

Katibu Mkuu huyo amesema Zanzibari inazalisha chakula cha Nafaka na Mbogamboga kwa asilimia 51, huku mchele ukiendelea kuzalishwa kwa kiwango kidogo na kuifanya serikali kuagiza kutoka nje ya nchi.

Amesema mpango wa Kilimo cha Umwagiliaji kwa upande wa Zanzibar bado haujaweza kuleta mafanikio makubwa ambayo yanahitajika kuanza kushughulikiwa ili kuhakikisha wakulima wa Zanzibari wanatumia teknoloaji hiyo ambayo ni msingi wa kuleta mapinduzi ya Kilimo.

Aidha, Katibu Mkuu huyo ameongeza kuwa mabadiliko ya tabia nchi yamekuwa yakichangia kuzorotesha maendeleo Zanzibar jambo ambalo linahitaji kudhibitiwa sambamba na upatikanaji wa zana bora za kisasa za kilimo hicho.

Sauti ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Kilimo, Maliasili, Mifugo na Uvuvi, Juma Ali Juma akielezea uboreshaji wa Kilimo