Jumatatu , 21st Dec , 2020

Jeshi la Polisi nchini kupitia kwa Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Liberatus Sabas, limetoa ripoti ya mwenendo wa hali ya usalama pamoja na tathmini ya matukio mbalimbali nchini kwa mwaka 2020 ambapo imeelezwa matukio yamepungua kwa kiasi kikubwa ukilinganisha na mwaka 2019.

Kamishna wa Operesheni na Mafunzo, Liberatus Sabas

Akizungumza na waandishi wa habari leo, Kamishna Sabas akiwa anatoa tathimini ya matukio mbalimbali kuanzia Januari hadi mwezi Novemba mwaka 2020,amesema vifo vitokanavyo na ajali, vimepungua kutoka 1329 mwaka 2019 hadi 1158 mwaka 2020, sawa na asilimia 12. 9.

“Jeshi la polisi limepata mafanikio makubwa yakupunguza matukio makubwa ambayo yalikuwa ni kero kubwa kwa wananchi hususani makosa ya kutumia silaha, mauji lakini pia ajali za barabarani, matukio ya kutumia silaha yamepungua kwa kiasi kikubwa tofauti na mwaka uliopita, mwaka 2019  kulikuwa kuna matukio 378 ya unyanganyi wakutumia silaha wakati mwaka huu kumekuwa na matukio 273” amesema Kamishna Sabas

“Matukio ya sasa mengi hayahusiana na matukio ya matumizi ya silaha kama zamani ni matumizi ya silaha nyingine kama panga, visu matumizi ya bunduki kwa asilimia kubwa sana yamedhibitiwa kwa kiwango kikubwa katika mikoa yote hapa Tanzania na hata matukio ya mauaji  mengi sasa hivi yanatokana na ushirikina, wivu wa kimapenzi na watu kujichukulia sheria mkononi” amesema Kamishna Sabas