Jumamosi , 13th Jul , 2019

Msanii wa muziki wa kizazi kipya hapa nchini Tanzania Barakah the Prince, ameeleza kuwa kwa sasa ana makazi nchini Kenya na amekataa suala la yeye kuitwa tapeli.

Barakah amesema hayo kupitia kipindi cha Friday Night Live "FNL" ya EATV, baada ya kuulizwa kama amehamia nchini Kenya.

"Kwakweli nina makazi Kenya, nina makazi hapa , sijakimbia Tanzania bado nina familia hapa, nina nyumba na ninaishi hapa. Nimeenda Kenya kwa sababu nataka kutanua wigo na soko la muziki wangu, nataka soko langu liwe kubwa kwa Afrika mashariki"

Aidha msanii huyo amezungumzia suala lililokuwa linaendelea mtandaoni la yeye kudaiwa na kuitwa tapeli kwa kusema, "hivo vitu vinatokea kwa sababu mimi ni mtu maarufu, sio mimi tu hata wanasiasa wakubwa, mabilionea nao wanaitwa matapeli, kwahiyo hamna kitu chochote kilichokuwa kinaendelea kati yangu mimi na ile stori iliyokuwepo" amesema.

Pia msanii huyo amedokeza ujio wa ndoa na mpenzi wake Naj itakayofanyika mwaka huu, baada ya wawili hao kuishi katika mahusiano kwa miaka mitano.