Jumatano , 17th Jul , 2019

Msanii wa muda mrefu kutoka tasnia ya Bongo Movie hapa nchini Tanzania Kulwa Kikumba maarufu kama "Dude", amefunguka kuhusu kauli ya mkuu wa mkoa wa Dar es salaam kuwa wasanii wengi ni ombaomba.

Kulwa Kikumba (Dude)

Dude amesema hayo leo kwenye mahojiano na EATV & EA Radio Digital, ambapo amekiri kuwepo kwa kundi la watu wanaojiita wakati wana kazi moja tu na muda mwingi wanatumia kufanya mambo yasiyofaa.

"Unajua kila aliyeshiriki kazi ya sanaa anajiita msanii, ila mimi naamini kwa wasanii wakongwe au ambao wamejikita zaidi kwenye sanaa hawawezi kuwa ombaomba, sio kuombaomba tu hata kuna mambo ya kijinga yanafanyika kwa wasanii tunaambiwa kuna wanaojiuza. Mtu akicheza filamu moja au akionekana kwenye tamthilia moja anajiita msanii ndio hao wanatupakazia watu wote".

Dude ameongeza kuwa anajua wasanii wanajiheshimu na wanauwezo wa kutafuta pesa zao. ''Napenda tu kumwambia mheshimiwa, wako baadhi ya watu wanaotuchafua, wanashiriki katika mambo ya ajabu kama kuvuta unga na wizi, kwa hiyo ndio hao wanatufanya sisi tuonekane wabaya."