Alhamisi , 7th Mar , 2019

Baada ya kushirikishwa kwenye wimbo wa Bam Bam wa Fid Q, Richi Mavoko na Big Jaman, Isha Mashauzi amekanusha tetesi zinazosema kwamba ataiacha taarabu na kuhamia katika muziki wa bongo fleva.

Isha Mashauzi

Isha amesema hawezi kuacha kuimba muziki wa taarabu kwa kuwa muziki wa taarabu ndo umemtangaza na kumfanya yeye kuwa na jina alilonalo hivi sasa akisema kuwa kwa upande wa Bongo Fleva kuna wanaofanya vizuri hivyo inabidi awaachie nafasi na sio kwamba anaogopa kushindwa. 

Hata hivyo Isha ameendelea kusema kwamba, "haikuwa rahisi kujiamini kufanya kazi ya Fid Q kwa kuwa ilikuwa mara yangu ya kwanza kufanya wimbo wa Bongo Fleva, nilikuwa nahofia japo niliingiza yale mashairi kwa siku moja na kwa muda mfupi kama masaa mawili hivi nikayaacha studio na kuamini chochote kitakacho tokea nitapigiwa simu".

"Lakini badae kuna mtu alikuja na kuniambia amesikiliza verse za wimbo huo nilizofanya na kunisifia kwamba ni nzuri na baada ya wimbo kutoka, Fid Q alinipongeza kuwa nilichokifanya kipo vizuri".

Pia Isha amemaliza kwa kusema anapenda kujifunza pale anapokosea na hapendi kiki kwa kuwa anaamini kwamba muziki wake pekee ni kiki tosha hivyo hawezi kutafuta kiki na kama kuna nyimbo yake ambayo anaambiwa ameimba vibaya huwa anakaa na kuisikiliza ili kuweza kuifanyia marekebisho badae.