Alhamisi , 22nd Sep , 2016

Kuelekea katika hatua ya fainali ya Dance100% zitakazofanyika siku ya Jumamosi wiki hii katika viwanja vya Don Bosco Oysterybay, vijana wametakiwa kutumia vipaji walivyonavyo kama kazi ili kuweza kujikimu kimaisha.

Wawakilishi wa makundi wakifanya ziara katika ofisi za Vodacom, Mlimani City Dar es Salaam

Meneja Uhusiano wa Vodacom Tanzania, Martina Nkurlu amesema, vijana hao wanatakiwa kuona kipaji walichonacho kuwa ni sehemu ya kazi ambayo itaweza kuwanufaisha hapo baadaye huku akiwataka watanzania waweze kujitokeza siku ya fainali ili kuweza kushuhudia vipaji vilivyopo.

Kwa upande wake Afisa Masoko wa EATV ambao ni waandaaji wa shindano hilo Brendansia Kileo amesema, wanategemea fainali zitakuwa na changamoto kubwa ya kiushindani kutokana na kila kundi kujiandaa vya kutosha ili kuweza kuibuka washindi wa shindano hilo.

Naye Afisa Masoko wa Kampuni ya Coca Cola ambao pia ni wadhamini wa shindano hilo Mariam Sezinga amesema, wanaamini vijana wengi wana vipaji, hivyo kwa upande wao pia wanaendelea kuvikuza ili kuweza kupata vijana wengi wenye vipaji hapa nchini.

Tags: