Jumatano , 25th Jan , 2017

Mwanamuziki wa nyimbo za injili Christina Shusho amefunguka na kuweka wazi ukweli wake kuwa siyo dhambi kwa mtoto wa kike kuvaa vazi la suruali kwa kuwa hilo ni vazi la kawaida ilimradi lizingatie maadili

Christina Shusho akiwa Kikaangoni

Mwanadada huyo mkali wa wimbo wa 'umenifanya ning'are' na nyingine nyingi amesema katika malezi aliyokulia alikuwa akiaminishwa kuwa suruali kwa mwanamke ni dhambi lakini alipojitambua alijaribu kuvaa vazi hilo na kugundua kuwa siyo dhambi.

"Mwanamke kuvaa suruali siyo dhambi, mimi mwenyewe nimekulia kwenye mazingira ambayo ilikuwa tabu kuvaa suruali
lakini inategemea na mazingira kama unaona utawakwaza watu ni bora uache"

Amefunguka hayo akiwa kwenye kipindi cha KIKAANGONI ambacho huruka LIVE kila Jumatano kupitia ukurasa wa Facebook wa EATV ambapo baadhi ya watu walihoji maamuzi yake ya kupendelea kuvaa suruali pamoja na hereni, ambapo alisema kwa Mungu hawaangilii mutu amevaa nini bali moyo wake na kwamba imani yake haimzuii yeye kuvaa hereni.

"Imani yangu haina shida na hereni wala kusuka, huko mbinguni haya mambo hayataangaliwa...." Alisema Christina.

Yafuatayo ni baadhi ya mambo usiyoyajua kuhusu Christina Shusho

Kuhusu baadhi ya mabinti kuvaa nusu utupu, Shusho alionekana kukerwa na uvaaji wa aina hiyo akidai kuwa siyo vizuri kuvaa kinyume na utamaduni wetu kama watanzania ambapo amesema "Kwa maadili ya kitanzania kuvaa nusu uchi kuna kundi fulani unawekwa ambalo siyo zuri... kwa mwanamke jinsi unavyoficha maumbile yako ndivyo unavutia zaidi kwa mwanaume, maana wanaume hutafuta vile vilivyofichwa, hakuna mwanaume anayetaka vilivyoachwa wazi"

Kuhusu maisha na familia yake, amesema kwa sasa ana umri wa miaka 40, ameolewa na ana watoto watatu, wakiwemo wawili wa kike na mmoja wa kiume. Mtoto wake mkubwa ana umri wa miaka 18 yuko kidato cha 5, wa pili miaka 15 yuko kidato cha 4, na wa tatu ana miaka 12 kidato cha pili. Mbali na hao amesema pia analea watoto wengine watatu

Shusho anasema kwa sasa mume wake ni mchungaji, hivyo na yeye sasa ni Mama Mchungaji na wana miaka 20 katika ndoa yao.

Alianza lini Uimbaji?: Anasema alianza kufanya kazi ya injili akiwa na umri wa miaka 16 baada ya kujitambua "Nimezaliwa katika familia ya watu waliookoka, lakini nikiwa na miaka 16 nilifanya maamuzi na kuamua kumtumikia Mungu"

Kuhusu elimu yake: Anasema alizaliwa na kusomea Kigoma hadi kidato cha nne, na baadaye alipata kozi ya masuala ya IT Jijini Dar es Salaam ambayo hata hivyo hakuimaliza, licha ya kuwa na malengo ya kuimalizia katika miaka ijayo.

Kwanini hana skendo? : Shusho amesema kujitambua na kutambua kazi yake ndiyo mambo yanayomfanya aendelee kufanya sanaa bila ya kuwa na skendo "Kujua unachokifanya, napenda nachokifanya, naheshimu sana kazi yangu"

Pia tazama video hii kumjua zaidi ikiwa ni pamoja na msanii wa bongo fleva anayemkubali, chakula asichojua kupika, n.k