Ijumaa , 6th Sep , 2019

Mchungaji wa Taifa 'Nabii Mashimo' ametolea ufafanuzi kifo cha aliyekuwa Rais wa kwanza wa nchi ya Zimbabwe na utabiri kuhusu vurugu za Afrika Kusini.

Mchungaji 'Nabii Mashimo'

Nabii Mashimo akizungumza na EATV & EA Radio Digital kuhusu kifo amesema kuwa,

"Nimepokea kwa masikitiko taarifa ya kifo cha aliyekuwa Rais wa Zimbabwe Robert Mugabe, ikumbukwe kwamba kifo chake nilikitolea unabii tangu tarehe 20/8/2017 nikiwa katika ubalozi wa Kenya, nilimwambia atengenezee nyumba yake na hatoweza kupata Urais kwenye uchaguzi wa mwezi wa 12 nchini Zimbabwe".

Nabii huyo ameendelea kueleza baada ya kutoa utabiri huo alikwenda ubalozi wa Zimbabwe uliopo Tanzania, ili kuomba kibali cha kwenda Ikulu ya nchi hiyo kumueleza marehemu Robert Mugabe, kuhusu maono ya unabii huo ambao umedhibitika leo hii.

Aidha Nabii Mashimo ametoa utabiri kuhusu vurugu zinazoendelea nchini Afrika Kusini ambapo amesema, Jicho la kinabii limeona maono ya Rais wa nchi hiyo na kila analolifanya kuhusu waafrika wanaoishi nchini kwake.

Pia amesema Mungu amemtuma amwambie Rais wa Afrika Kusini kuwa afanye toba, amalize ghasia hizo ndani ya siku 3 la sivyo damu zilizoangamia zitakuwa juu yake na atatolewa madarakani mapema sana.