Jumatano , 9th Jan , 2019

Familia moja huko Naivasha nchini Kenya, imeshangaza umma baada ya kuufukua mwili wa mtoto wao aliyefariki wiki iliyopita, kwa lengo la kumuombea afufuke.

Mama wa mtoto huyo ambaye alifariki kwa ajali akiwa na mwaka mmoja tu, aliita wachungaji na kisha kwenda kufukua maiti hiyo ambayo ilikwisha zikwa, na kuanza kufanya maombi ya kumfufua, jambo ambalo liliwashangaza wakazi wa eneo hilo waliodhani ni imani au ushirikina, na kuamua kuita polisi.

Jeshi la Polisi katika eneo la Naivasha lilifika eneo husika na kuwatia nguvuni wahusika wa tukio hilo, wakisema kwamba wamewakamata kwa kitendo cha kufukua mwili wa marehemu bila kibali cha serikali.

“Hatuna shida na imani, shida yetu ni tendo ambalo limefanyika, kwamba walifukua mwili bila kuwa na idhini ya serikali ya kufukua mwili, hivyo tunawashukuru watu wa eneo hili kwa taarifa, na pia poleni, sasa tunaangalia labda tutayafanya haya mazishi tena”, alisikika Mkuu wa Polisi Naivasha akiwaambia wakazi waliofika kushuhudia tukio hilo lililowaacha midomo wazi.