Jumanne , 19th Jun , 2018

Afisa habari wa klabu ya Simba, Haji Manara amefunguka kuhusu uwepo wa kocha Lechantre ndani ya timu hiyo mabingwa wa Ligi kuu Tanzania Bara, ambapo dalili zinaonesha kuwa hana nafasi tena.

Akizungumza na eatv.tv Manara amesema kuwa Pierre Lechantre amemaliza mkataba na klabu hiyo huku akionesha wasiwasi mkubwa kwa kocha huyo kama ataweza kuendelea na wekundu hao wa Msimbazi au la.

"Lechantre amemaliza mkataba na sisi lakini sijui kama ataendelea au la!, kama kutakuwa na haja na uhitaji ataongezewa mkataba ila sioni kama kuna tarajio hilo" amesema Manara.

Manara ameongeza kuwa “kuhusu usajili baada ya kuwasajili akina Salamba na wengine bado tutaongeza mashine mbili za kigeni na tutawatambulisha muda siyo mrefu" ameongeza Manara.

Lechantre alijiunga na Simba katikati mwa raundi ya kwanza ya Ligi kuu akichukua nafasi ya Mcameroon Joseph Omog aliyetupiwa virago baada ya kichapo kutoka kwa Green Warrious.