Jumamosi , 2nd Oct , 2021

Ligi Kuu Tanzania Bara imeendelea siku ya leo kwa michezo mbali mbali ambapo Azam FC imekumbana na kipigo cha magoli 2-1 kutoka kwa Polisi Tanzania katika dimba la Ushirika Moshi.

Kocha wa Azam Fc, George Lwandamina wakizungumza jambo mazoezini

Polisi walitangulia mapema dakika ya 23 kupitia kwa Kassim Shaban, kabla ya Iddi Selemani kusawazisha katika dakika ya 29 na baadaye katika dakika ya 40 Adam Adam alifunga goli la ushindi kwa upande wa Polisi Tanzania na kufanya mchezo kuwa 2-1 mpaka dakika ya 90.

Akizungumza mara baada ya mchezo kumalizika, kocha msaidizi wa Azam Fc, Vivier Bahati amesema wameadhibiwa kutokana na makosa ya safu ya ulinzi huku akionekana kutofurahishwa na kutokupatikana kwa mabao.

Naye kocha mkuu wa Polisi Tanzania, Malale Hamsini amesema wanapata matokeo mazuri kwakuwa wamesajili vijana ambao wana njaa namafanikio.

Kwa matokea hayo Azam wanasalia na alama moja baada ya michezo miwili ya ligi kuu lakini Polisi Tanzania wamekamata usukani wakiwa na alama sita baada ya ushindi katika mechi zao zote mbili.

Mchezo mwingine uliopigwa leo Coastal Union wakiwa kwenye dimba lao la Mkwakwani, walitoshana nguvu na KMC kwa kutoa sare 0-0 hivyo kuifanya timu hiyo ya Tanga kukusanya jumla ya 2 huku KMC wakiwa na alama moja baada ya michezo miwili.