Alhamisi , 8th Nov , 2018

Mwanafunzi wa sekondari jijini Dar es salaam ambaye ni mchezaji wa timu ya taifa ya kikapu ya U18,  Atiki Ally Atiki amefanikiwa kupata udhamini wa Kwenda kusoma elimu ya juu ya sekondari nchini Canada kwenye shule ya Themes Valley district school Board.

Mchezaji wa kikapu, Atiki Ally Atiki

Atiki amepata udhamini huo kupitia taasisi ya JUCO Advocates ambayo ilikuja hapa nchini kwa mualiko wa kocha wa timu ya Taifa Matthew McAllister kupitia mafunzo maalumu yaliyoyafanyika mwezi Agosti 2017.

Atiki Anatarajiwa kuanza masomo Februari mwakani na katika kipindi kilichosalia kabla ya kujiunga na shule hiyo, atakua akifanya mazoezi na kucheza katika kituo cha, London Basketball Academy iliyopo katika mji wa Ontario, Canada. Anatarajiwa kumaliza masomo na kupata secondary school diploma mwezi wa tisa mwaka kesho. 

Safari ya Atiki katika Mpira wa kikapu ilianzia Mwanza miaka miwili iliyopita alipohamia Dar Es salaam na kusoma shule ya msingi Gerezani huku akifanya mazoezi katika timu ya JMK PARK Academy. Amecheza kwa Muda Mfupi kwenye timu ya Jogoo na baadae kupandishwa kucheza kwenye timu ya Kwanza ya Vijana baada ya kufanya vizuri.

Atiki ni mchezaji wa timu ya Taifa ya Vijana U18 ambapo mwaka huu alishriki kwenye mashindano ya zone 5 na akachaguliwa kuwa miongoni mwa wachezaji 5 bora katika shindano hilo.

Pia alishiriki katika michuno ya kikapu ya Sprite Bball Kings iliyofanyika mwezi Juni na Julai mwaka huu inayoandaliwa na EATV, ambapo alikuwa mchezaji wa Portland.
Katika michuano hiyo, Portland ilifanikiwa kucheza hatua ya fainali dhidi ya Mchenga Bball Stars ambapo Portland ilifungwa katika michezo yote mitatu.

London Basketball Academy ambayo Atiki atajiunga nayo, inashiriki kwenye mashindano mbalimbali nchini Canada na Marekani.