Jumanne , 30th Jun , 2020

Ligi kuu ya soka England pamoja na kombe la ligi nchini humo (EFL) kwa kushirikiana na chama cha wachezaji wa kulipwa (PFA), wamekuja na mpango wa kuboresha uwezo kwa makocha weusi, wenye asili ya Asia na wanaotoka nchi nyingine ambazo hazijapiga hatua kwenye soka.

Nembo za Premier League, PFA na EFL

Kwa mujibu wa kocha wa klabu ya Doncaster Rovers ambaye ni mshauri wa mpango maalumu wa watu weusi kwenye Premier League, Darren Moore amesema utaratibu huo utaanza msimu ujao wa 2020/2020.

Utaratibu kamili wa mpango huo kwa msimu ujao ni kuwapa nafasi makocha sita wanaotoka kwenye nchi za (BAME), kujumuika kwenye benchi la ufundi msimu mzima kwenye vilabu kadhaa vinavyoshiriki kwenye Kombe la Ligi (EFL).

Hadi sasa ni makocha 6 tu wanaotoka nchi za BAME ambao wanafundisha kama makocha wakuu katika vilabu 91 vya Premier League na EFL, hivyo lengo la mpango huo ni kuongeza idadi.

Kocha wa Wolverhampton Wanderers F.C Nuno Espirito Santo ndio kocha pekee anayewakilisha watu weusi, Asia na minority ethnic (BAME) kwenye Premier League.

VIGEZO NA MASHARTI

Mpango huo ambao unafadhiliwa na Chama cha soka England (FA) pamoja na PFA, unamtaka kocha awe na leseni B ya ukocha inayotambulika na shirikisho la soka barani Ulaya (UEFA).

Pia kocha anayeomba kuingia kwenye mpango huo anatakiwa kuwa tayari ameshaanza kushughulika na mafunzo ya kupata leseni A ya ukocha ya UEFA.

Pia awe ameshiriki (FA Advanced Youth Award) na kupitia majaribio kadhaa katika vilabu tofauti tofauti. 

Aidha Mtendaji kuu wa Premier League Richard Masters amesisitiza kuwa mpango huu ni fursa kwa makocha kupata nafasi zaidi za ajira.