Jumatano , 14th Jan , 2015

KOCHA wa Klabu ya Simba, Goran Kopunovic amesema hivi sasa hafikirii ushindi alioupata wa Kombe la Mapinduzi uliomalizika hapo jana bali anachotazamia ni Michuano ya Ligi Kuu katika mechi zilizobakia.

Akizungumza na East Africa Radio, Goran amesema, licha ya ushiriki na ushindi wa michuano hiyo, lakini anaamini Zanzibar walienda kwa ajili ya maandalizi ya Ligi Kuu ambapo anaamini wachezaji wake watafanya vizuri katika Ligi zilizobakia.

Goran amesema, katika mechi za Ligi Kuu anaamini mchezo utakuwa ni mgumu kutokana na kila timu kujiandaa kwa ajili ya kuweza kushinda lakini anaamini amekuja kwa ajili ya kubadilisha kikosi na kiweze kufanya vizuri katika Ligi hiyo.

Kwa upande wake Mlinda Malango wa Klabu hiyo, Ivo Mapunda amesema, mashindano ya Muungano yamewaandaa vizuri kwa ajili ya mechi ya Jumamosi Dhidi ya Ndanda na wanaamini mazoezi ya Kocha yatasaidia wachezaji kuweza kufanya vizuri katika mechi mbalimbali za Ligi Kuu.

Timu ya Simba imewasili leo jijini Dar es salaam ikitokea visiwani Zanzibar, ambapo imeelekea Mtwara kwa ajili ya maandalizi ya Mechi dhidi ya Ndanda FC, mchezo utakaochezwa uwanja wa Nangwanda, mjini Mtwara.