Jumatatu , 8th Jun , 2015

Mashindano ya Klabu Bingwa ya Taifa yanatarajiwa kuanza Juni 10 mwaka huu mkoani Kigoma kwa kushirikisha vilabu mbalimbali vya ngumi hapa nchini.

Akizungumza na East Africa Radio, Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi nchini BFT, Makore Mashaga amesema, maandalizi kwa ajili ya pambano hilo yanaendelea ambapo vilabu shiriki vimeshawasili Kigoma kwa ajili ya kushiriki mashindano hayo.

Mashaga amesema, wameamua kupeleka mashindano hayo mkoani Kigoma ili kuweza kuukuza mchezo huyo katika mikoa yote hapa nchini.

Mashaga amesema, katika mashindano hayo watachagua wachezaji watakaofanya vizuri wataungana na wachezaji wanaounda timu ya Taifa ili kukiimarisha kikosi hicho kinachotarajiwa kushiriki mashindano ya All African Games Septemba mwaka huu pamoja na ubingwa wa Dunia yatakayofanyika nchini Qatar na Mashindano ya Olimpiki 2016.