Jumamosi , 16th Oct , 2021

Kocha wa klabu ya Yanga, Mtunusia Mohammed Nasreddine Nabi amesema anajua namna ya kuwakabili wapinzani wake klabu ya KMC ambayo wanataraji kucheza nayo Jumanne ya Oktoba 19, 2021 Songea Mjini, Mkoani Ruvuma.

(Kocha wa Yanga, Mohammed Nasreddine Nabi akiwa anatoa maelekezo mkwa mchezaji Feisal Salum wakiwamazoezini)

Nabi ameyasema hayo wakati kikosi chake kikiwa kinafanya maandalizi ya mwisho wikiendi hii kabla ya kusafiri leo Oktoba 16, 2021 kuelekea Mkoani Ruvuma.

Kocha huyo amesema, "Tunafanya mazoezi ya aina mbali mbali, kwa sasa tumezingatia zaidi kujenga stamina. Wachezaji wanatakiwa kuwa imara. Ligi ni safari ndefu, wanatakiwa wawe katika kiwango cha juu cha kushindana kuanzia mwanzo hadi mwisho wa msimu"

"KMC ni moja ya timu ambazo wachezaji wake wanatumia nguvu, ninajua namna ambavyo tutawakabili. Naamini tutapata kile ambacho tunakihitaji kama timu" Amesema Nabi.

Vile vile Nabi akagusia umuhimu wa kupata ushindi kwenye mchezo huo kwa kusema, "Tunahitaji ushindi katika mechi hiyo ili kutuweka kwenye nafasi nzuri, tukipata matokeo mazuri yatakuweka kwenye nafasi nzuri ya kuelekea katika maandalizi ya kuwakabili Azam, mechi zote zinahitaji kuwa na kikosi imara"

Yanga inataraji kujitupa dimbani siku ya Jumanne Oktoba 19, 2021 saa 10:00 jioni kwenye uwanja wa Maji Maji uliopo Songea Mjini, Mkoani Ruvuma kisha kurejea Dar es Salaam kujiandaa kucheza dhidi ya klabu ya Azam.

Baada ya michezo miwili ya Ligi kuu kuchezwa, Yanga ipo nafasi ya pili ikiwa na lama 6 baada ya kuwafunga Biashara United Mara na Kagera Sukari kwa 1-0 kwenye michezo hiyo ilhali KMC ni wa 15, wapili kutoka mkiani akiwa na alama 1.