Alhamisi , 8th Nov , 2018

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Magufuli ameandika barua ambayo itapelekwa kwa Waziri Mkuu wa Israel, Israel Benjamin Netanyahu kwaajili ya shukrani kwa kutambua mchango wa taifa hilo kwa Tanzania.

Rais Magufuki (kushoto) na Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu

Rais Magufuli amesema hayo leo Novemba 8, alipokutana na timu ya wataalamu wa matibabu ya moyo kutoka nchini Israel na Marekani, Ikulu Jijini Dar es salaam, wataalam hao wanashirikiana na Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete.

"Nimeandika barua ambayo nitakukabidhi Balozi, umpelekee Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu inayoeleza namna ninavyokubali utendaji kazi wake, najua hii barua itamfikia ili kuonesha kazi nzuri mliofanya," amesema Rais Magufuli.

"Niwaombe Madaktari na Wataalamu kutoka Israel mkija msije tu kwa masuala  ya Udaktari siku nyingine mnaweza mkaja kwa masuala ya kufurahi,  mnaenda Serengeti National Park, Ngorongoro na maeneo mengine ambayo ni  ya kuvutia".

Madaktari hao zaidi ya thelathini wamekuja nchini kwaajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto 51 katika Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete, Hospitali ya taifa ya Muhimbili.