Jumatatu , 9th Sep , 2019

Meneja wa klabu ya Simba, Patrick Rweyemamu amesema kuwa klabu yake imepata hasara kwa kiasi chake baada ya kuondolewa katika hatua ya awali ya Klabu Bingwa Afrika.

Patrick Rweyemamu

Ameyasema hayo katika mazoezi ya timu hiyo yanayoendelea Jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kujiandaa na ratiba ya Ligi Kuu Tanzania bara (VPL).

Rweyemamu amesema kuwa hasara inaweza kuwepo au isiwepo kwa klabu hiyo kutokana na namna uwekezaji ulivyofanyika, ambapo amebainisha kuwa uwekezaji mkubwa ulikuwa katika usajili pamoja na gharama za uwekezaji.

"Gharama inaweza ikawepo au isiwepo kwa sababu msimu uliopita tulikuwa tunasafiri, posho, bonasi, visa pamoja na mahitaji mengine", amesema Rweyemamu.

"Kwa upande mwingine tumepoteza hela pia, tulikuwa tunategemea kule kama chanzo cha mapato kwa sababu tulipofika robo fainali tulipata zaidi ya  Dolla laki 6 na elfu 50 kwahiyo nao ulikuwa ni mtaji kwetu na sasa hatutoupata. Ni changamoto lakini lazima tupambane", ameongeza.

Simba ilitolewa katika hatua ya awali ya michuano ya Klabu Bingwa Afrika na klabu ya UD du Songo ya Msumbiji baada ya kutoka sare ya kufungana bao moja kwa moja katika uwanja wa taifa Jijini Dar es Salaam, ambapo katika mchezo wa kwanza nchini Msumbiji timu hizo zilitoka suluhu ya bila kufungana.