Ijumaa , 14th Sep , 2018

Kiungo wa Barcelona na timu ya taifa ya Croatia, Ivan Rakitic amemtoa nyota wa klabu yake, Lionel Messi katika mbio za kuibuka na ushindi wa tuzo kubwa za dunia msimu huu na kumpa nafasi kubwa nahodha wake wa timu ya taifa, Luka Modric.

Luka Modric (kushoto) na Ivan Rakitic

Rakitic anaamini kuwa katika ushindani wowote ambao Messi atashindanishwa na Modric, nafasi kubwa itakuwa kwa Modric kuweza kushinda tuzo hiyo.

Mpaka sasa, Luka Modric ameshinda tuzo ya mchezaji bora wa michuano ya kombe la dunia baada ya kuifikisha timu yake ya taifa katika fainali na tuzo ya mchezaji bora wa Ulaya msimu wa 2017/18.

Messi ameachwa katika listi ya wachezaji wanaowania tuzo ya mchezaji bora wa dunia wa FIFA, ambapo waliotajwa katika listi hiyo ni, Mohamed Salah, Cristiano Ronaldo na Luka Modric.

“Kama kuna tuzo za kushindanisha baina ya wachezaji msimu huu, basi Messi hawezi kushinda tuzo yoyote. Hakuna shaka kuwa msimu huu tuzo itakwenda kwa Luka Modric”, amesema Rakitic.

“Haitonishangaza endapo atashinda kwa kura nyingi, huu umekuwa ni mwaka wake, kama Messi sio bora basi Modric anastahili zaidi na ninafuraha kuona anafanikiwa”, ameongeza.

Mafanikio mengine ya Luka Modric mwaka huu ni kuiongoza Real Madrid kushinda ubingwa wa klabu bingwa ulaya mbele ya Liverpool mwezi Mei.