Sintofahamu ya TFF na Kapombe
Kwa mujibu wadau mbalimbali wa soka, inawatia wasiwasi mkubwa kuziamini taarifa za moja kwa moja kutoka kwa kiongozi yoyote wa shirikisho hilo kutokana na siku za hivi karibuni mmoja wa kiongozi wake kutoa taarifa kuwa Kagera Sugar imeporomoka ligi na baadaye kukanushwa na kiongozi mwingine, pia taarifa nyingine ni juu ya majeraha ya mlinzi wa Simba, Shomari Kapombe.
Suala la Kagera Sugar kushuka daraja, mara baada ya ligi kumalizika, Afisa Habari wa TFF, Cliford Ndimbo alikaririwa kuwa timu hiyo ndiyo itakayoungana na African Lyon kushuka daraja moja kwa moja, lakini baada ya muda mfupi, Mkurugenzi wa Bodi ya Ligi, Boniface Wambura alikanusha taarifa hiyo na kusema kwamba kuna kiongozi alifanya uzembe wa kuweka taarifa zisizo sahihi katika msimamo wa ligi. Aliirudisha Kagera Sugar katika Playoff na kuahidi kutoa adhabu stahiki kwa kiongozi aliyehusika katika upotoshaji huo.
Jana, Juni 3 pia kumekuwepo na mkanganyiko juu ya taarifa ya majeraha ya mlinzi wa Simba na timu ya taifa, Shomari Kapombe ambaye aliitwa katika kikosi cha Taifa Stars kinachokwenda nchini Misri. Afisa Habari wa TFF alikaririwa akisema kuwa Shomari amejitonesha majeraha katika mazoezi na timu ya taifa, ambapo hali yake inaangaliwa kama ataweza kuwa fiti kabla ya michuano.
Baada ya muda mfupi, Kapombe alikanusha taarifa hiyo akisema kuwa hajajiunga na kambi ya timu ya taifa na anaendelea na mazoezi yake binafsi kama alivyoagizwa kocha wake wa Simba, huku akiwataka watu kuacha kusambaza taarifa hizo za uongo.
Kutokana na mikasa hiyo, inaonesha kuwa kuna uwasilishaji mbovu wa taarifa kutoka TFF, jambo ambalo limepelekea kuwepo kwa mashaka kwenye ukweli wa kila taarifa ambayo itakuwa inatoka kwenye shirikisho kwenda kwa wadau wa soka nchini.