Jumamosi , 7th Jul , 2018

Timu ya Kikapu ya Portland kutoka Kinondoni imeongoza mbio za kuelekea robo fainali ya Sprite Bball Kings 2018 baada ya kushinda kwa vikapu 126 dhidi ya 54 vya Mbezi Beach KKKT kwenye mchezo uliopigwa kwenye viwanja vya Airwing Ukonga jioni ya leo.

Wachezaji wa timu ya Portland

Kwa matokeo hayo Portland imeongoza kwa tofauti kubwa ya pointi ukilinganisha na timu zingine tatu zilizoshinda mechi zake za hatua ya 16 bora leo na kutinga robo fainali.

Mechi tatu zingine zilizopigwa leo pale Airwing Ukonga ni ile ya DMI ambayo imeilaza Fast Heat kwa vikapu 113 dhidi ya 64, hivyo kukaa katika nafasi ya pili kwa kushinda vikapu vingi leo huku ikikata tiketi ya robo fainali ya Sprite Bball Kings msimu wa 2018.

Flying Dribblers nao hawakuwa nyuma ambapo waliibuka na ushindi dhidi ya Ukonga Hitmen wakiwajaza vikapu 87 kwa 63. Vikapu hivyo vimewapa kibali cha robo fainali wakisubiri droo tu kujua watacheza na nani.

St. Joseph nao wamehakikisha wanatinga hatua ya robo fainali baada ya kuwafunga Air Wing vikapu 98 kwa 78. Kesho hatua ya 16 bora itaendelea kwa mechi nne kupigwa kwenye uwanja wa Bandari Kurasini hakutakuwa na kiingilio kama ilivyokuwa leo Airwing Ukonga.