Alhamisi , 15th Dec , 2016

Benchi la ufundi la klabu ya Ndanda FC limesema kuwa timu hiyo imechoka kunyanyaswa na Simba SC, na sasa imejipanga kuifanyia miujiza katika mchezo wa kwanza wa mzunguko wa pili wa ligi kuu Tanzania Bara utakaopigwa Jumapili, Desemba 18, mwaka huu.

Mechi ya mzunguko wa kwanza kati ya Simba na Ndanda katika dimba la Taifa, Ndanda ilichapwa 3-1 na Simba

Benchi hilo limesema kuwa kikosi chake kimejiandaa vizuri na kinaendelea na mazoezi kuhakikisha kuwa mnyama anakufa siku ya Jumapili, na kwa mara ya kwanza kuweka rekodi ya kuifunga timu hiyo ambayo imekuwa ikiinyanyasa kwa kuifunga katika mechi zote ambazo wamekutana.

"Simba asitarajie mteremko, tumechoka kupata matokeo ya kufungwa na Simba, tumechoka kunyanyaswa na Simba, safari hii lazima mnyama achinjwe katika dimba la Nangwanda Sijaona" Amesema mmoja wa viongozi wa klabu hiyo.

Kwa upande wao Simba, tayari wako njiani na wanataraji kutua Mtwara muda wowote tayari kwa mtanange huo wa Jumapili wakiwa na kikosi chao kizima.

Katika mchezo wa mzunguko wa kwanza, Simba iliifunga Ndanda mabao 3-1 katika dimba la Taifa Dar es Salaam, lakini klabu hiyo ya Mtwara iliweza kuisimamisha Yanga kwa kuilazimisha sare ya 2-2 katika dimba la Nangwana Sijaona, Mtwara