Jumamosi , 9th Dec , 2017

Timu ya taifa ya kandanda ya Zanzibar (Zanzibar Heroes) imekuwa timu ya kwanza kufuzu hatua ya fainali ya CECAFA Senior Challenge baada ya kutoka suluhu na Kenya jioni hii.

Mchezo huo umemalizika jioni hii kwenye uwanja wa Kenyatta uliopo County ya Machakos ambapo Zanzibar Heroes imeilazimisha suluhu ya 0-0 timu ya taifa ya Kenya Harambee Stars.

Zanzibar Heroes imefuzu hatua hiyo baada ya kushinda michezo miwili dhidi ya Rwanda na Kilimanjaro Stars na kutoka sare moja ya leo dhidi ya Kenya, hivyo kuongoza kundi A.

Zanzibar Heroes sasa imefikisha alama 7 na kufuzu hatua hiyo ikifuatiwa na Kenya yenye alama 5 ambayo itasubiri matokeo yake ya mchezo wa mwisho dhidi ya Kilimanjaro Stars.

Mapema mchana leo timu ya taifa ya Tanzania Bara (Kilimanjaro Stars) imetolewa katika michuano hiyo baada ya kufungwa mabao 2-1 na timu ya taifa ya Rwanda.