Ijumaa , 7th Oct , 2016

Kikosi cha Mbeya City kinatarajia kushuka dimbani leo katika Uwanja wa Sokoine jijini Mbeya katika mchezo mwingine wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania bara dhidi ya wageni Stand United kutoka mkoani Shinyanga kikiwa bila nyota wake kadhaa wa safu ya ulinzi.

Mbeya City

Afisa Habari wa Mbeya City Dismas Ten amesema, maandalizi kuelekea mchezo huo yamekamilika na City itashuka dimbani ikiendelea kuwakosa nyota wake wawili wa safu ya ulinzi, Haruna Shamte na Sankhani Mkandawile ambao waliumia katika mchezo wa ugenini dhidi ya JKT Ruvu uliochezwa Mlandizi mkoani Pwani na City kufungwa bao 2-0.

“Kwenye kikosi tunaendelea kuwakosa Haruna na Sankhani na hii ni kwa sababu bado wanauguza majeraha lakini taarifa njema ni kuwa mlinzi Rajab Zahir amerejea kikosini kuongeza nguvu baada ya kushindwa kumaliza dakika 90 za mchezo dhidi ya Mwadui kufutia maumivu ya kifungo cha mguu, na madaktari wamethibitisha kuwa yuko safi na tayari kwa mchezo wa kesho”, amesema Ten.