Alhamisi , 18th Oct , 2018

Klabu ya soka ya Azam FC ambayo kesho itashuka dimbani kucheza na African Lyon, lakini tayari imeshaanza kuwaza mchezo wake dhidi ya Singida United, utakaopigwa kwenye uwanja wa Namfua mjini Singida, uwanja ambao Azam FC haijawahi kuchezea.

Azam FC juu na Singida United chini

Akiongea leo kuelekea mchezo wa kesho fisa habari wa Azam FC, Jaffar Idd Maganga amesema, mchezo wa kesho ni muhimu na ni wa ushindani, kutokana na uwezo wa African Lyon huku wakiendelea kutazama mechi zijazo ambazo watacheza nje ya uwanja wao ikiwemo ya ile ya Singida United.

''Tunacheza mchezo wetu dhidi ya African Lyon ambao ni wa nyumbani katika mechi za hivi karibuni na baada ya mchezo huu, tutakwenda kucheza na JKT Tanzania kisha kusafiri kwenda kucheza na Singida United kwa mara ya kwanza kwenye uwanja wao wa Namfua'', amesema Jaffar.

Azam FC haijawahi kucheza na Singida United wakiwa kwenye uwanja wao baada ya kucheza mechi ya mzunguko wa kwanza kwenye uwanja wa Jamhuri Dodoma ambao Singida walikuwa wanautumia kama uwanja wa nyumbani wakati Namfua ukiwa kwenye matengenezo.

Mbali na hilo Jaffar amesema timu hiyo imejiandaa vyema ikiwa na nguvu mpya kutoka kwa mchezaji wake Bruce Kangwa ambaye alikuwa kwao Zimbabwe baada ya kupata msiba mwezi mmoja uliopita.

Jaffar amebainisha kuwa tayari wachezaji waliokuwa kwenye timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars), wamesharejea kikosini kwaajili ya michezo ya ligi kuu. Wachezaji wa Azam FC waliokuwa Stars ni Agrey Morris, David Mwantika, Mudathir Yahya na Yahya Zayd.